BUNGE LAPITISHA KWA KISHINDO BAJETI YA MADINI TSH BILIONI 224.98 KWA MWAKA 2025/2026*
▪️ Maabara ya Kisasa ya Madini kujengwa Dodoma.
▪️ Helikopta kununuliwa na kufungwa vifaa maalum kwa ajili ya utafiti.
▪️ Wachimbaji Wadogo, Wanawake na Vijana ni sehemu ya Kipaumbele.
Dodoma.
Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kauli moja wamepitisha kwa kishindo Bajeti ya Ofisi ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2025/26 yenye takribani Shilingi bilioni 224.98 kwa ajili ya wizara na taasisi zilizo chini yake kutekeleza majukumu yake.
Bajeti hiyo iliyopitishwa kwa uungwaji mkono mkubwa kutoka kwa wabunge, inalenga kuendeleza utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika Sekta ya Madini pamoja na kuimarisha utoaji wa huduma na utendaji kazi wa wizara na taasisi zake.
Awali, Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde akiwasilisha Hotuba ya Mpango wa Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha wa Serikali wa 2025/2026 leo Mei 02, 2025 Bungeni Jijini Dodoma, ameeleza Bunge kuwa kiasi hicho ni kwa ajili ya kuwezesha Wizara ya Madini na taasisi zake kutimiza majukumu na wajibu wao.
“Mheshimiwa Spika, ili Wizara iweze kutekeleza majukumu na malengo yaliyopangwa ikiwemo ukusanyaji wa maduhuli ya shilingi 1,405,537,268,755.00 (Trilioni 1.4) naomba Bunge lako Tukufu liridhie na kupitisha makadirio ya shilingi 224,984,150,000.00 kwa ajili ya matumizi ya Wizara na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026” ameeleza Mavunde.
Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, mchanganuo wa bajeti hiyo, Shilingi 124,604,788,000.00 (Bilioni 124.6) sawa na asilimia 55.38 ya bajeti yote imetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambayo inalenga kuleta tija na kuchochea ukuaji wa sekta ya madini hapa nchini.
Ameeleza kuwa, Shilingi 100,379,362,000.00 (bilioni 100.3) sawa na asilimia 44.62 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ambapo kati ya hizo, Shilingi 24,268,585,000.00 zimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi (PE) huku Shilingi 76,110,777,000.00 ikitengwa kwa ajili ya matumizi mengineyo (OC) ya Wizara pamoja na taasisi zilizo chini yake.
Kupitishwa kwa bajeti hiyo kwa kauli moja kunatoa ishara ya dhamira ya Serikali kuendelea kuwekeza kwa nguvu.
TEITI Office Dodoma
Postal Address: Government City, Mtumba, S.L.P 361 Dodoma, Tanzania Email: info@teiti.go.tz
Telephone: +255 26 2610760
Mobile:
Email: info@teiti.go.tz
Copyright ©2016 TEITI . All rights reserved.